latest Post

TABIA KUMI ZA KUIMARISHA AFYA YAKO

Katika mazingira tunayoishi sasa  changamoto za kiafya zimekuwa nyingi sana , watu kuumwa mara kwa mara kutokana na magonjwa mbalimbali pamoja na lishe duni hivyo kupelekea kupunguza nguvu kazi katika uzalishaji.Jambo kubwa ambalo  limewagharimu watu wengi ni ukosefu wa elimu bora juu ya afya na lishe, utaratibu wa ulaji na mwenendo wa maisha umesababisha watu wengi kutozingatia sana swala hili bali watu wengi wameweka mawazo yao katika kutafuta pesa, sio jambo baya  kutafuta pesa ni jambo zuri lakini utafaidi vipi matunda ya kazi yako kama  una afya dhaifu?

Hivyo ni vyema tukaweka mawazo yetu pia katika kuboresha afya zetu ili tufaidi matunda ya kazi zetu(weka afya yako katika sehemu ya vipaumbele vyako).Hivi unafahamu kuna watu  ndani ya mwaka mzima hawajaumwa wala kwenda hospitali kupatamatibabu?, lakini pia kuna wengine kila mwezi inawalazimu kwenda hospitaliili kupata matibabu ya afya zao. Tofauti ya watu wa namna hii ni kuwa na vipaumbele katika kuboresha afya zao kila siku.Makosa madogo madogo ya kiafya watu wengi wanayofanya kila siku matokeo yake yanaweza uonekana miaka  miwili au mitatu ijayo.Hivyo kama huoni sasa tarajia ipo siku yataonekana tu.

Leo nataka nikupe mambo Kumi ambayo ukifanya kwa kila wiki afya yako itaimalika na kuwa mtu mwenye afya bora.Kumbuka ukiwa na afya bora ni rahisi kula matunda ya kazi yako nje ya hapo watafaidi watu wengine wakati wewe unaughulia tu.


1.KUWA MTU WA FURAHA 


Kuwa mtu wa furaha ni jambo muhimu sana katika kuboresha afya ya mwili wako.kama ulikuwa ufahamu basi tambua leo kuwa na furaha ni dawa tosha katika kuimarisha afya yako.furaha na afya njema  huwa vinaendana pamoja, tafiti za kisayansi zinaonyesha  kuwa na furaha huleta faida katika afya ya moyo na kuboresha mfumo wa kinga mwilini na kuishi maisha marefu.Anza leo kuwa mtu wa furaha kwa sababu  furaha haiuzwi ni uamuzi wako.Ukiamua kuwa mtu wa furaha hakika utaona mabadiliko katika afya yako.
SOMA:Furaha inavyoboresha afya yako

2.KUFANYA MAZOEZI


Kufanya mazoezi ni muhimu sana katika kuboresha afya ya mwili wako.Zipo faida nyingi unapoamua kuwa na tabia ya kufanya mazoezi.Faida kama kuwa na muonekano mzuri,kupata hamu ya kula,kuupa mwili nguvu pamoja na kuifanya akili yako ifanye kazi vizuri.Ni vyema ukafanya mazoezi kila wiki hata kama ni kwa dakika 15 kila siku,utapata faida kubwa katika afya ya mwili wako.
Soma:Mazoezi 6 Muhimu unayoweza fanya asubuhi

3.KUNYWA MAJI YA KUTOSHA

Kunywa maji ya kutosha kuna faida nyingi. Tukichukulia kunywa maji ya kutosha ni mithili biashara kati ya wewe na afya yako, biashara hii inalipa.Baadhi ya faida ni Kusaidia mmeng’enyo wa chakula,Kuboresha afya ya ngozi,Dawa ya maumivu ya kichwa,Kuboresha hali ya viungo na misuli na Kupunguza uwezekano wa kupata baadhi ya magonjwa.Unashauriwa kunywa lita mbili mpaka tatu  za maji kila siku.


4.KUFANYA TAHAJUDI(MEDITATION)


Hali ya kuwa na msongo wa mawazo limekuwa jambo la kawaida kwa watu wengi na kupelekea kudhorota kwa afya zao.Njia moja wapo wa kutatua tatizo hili ni kufanya mazoezi ya tahajudi au kwa kiingereza tunaita meditation.Mazoezi haya huwa na faida kubwa sana katika kuboresha afya yako kwani husaidia kuleta furaha,kutibu matatizo mengi ya kisaikolojia,kuimarisha mfumo wa kinga mwilini na pia kuondoa mawazo hasi katika akili yako.Unashauriwa kufanya mazoezi haya angalau kwa dakika tano kwa siku.
SOMA Maana na Faida za Mazoezi ya Tahajudi katika Afya yako

5.KULA MATUNDA


Matunda ni chakula pia matunda ni dawa katika mwili wako kwani yanauwezo wakutibu magonjwa mbalimbali  na kukulinda dhidi ya magonjwa katika mwili wako.Kama huna utaratibu wa kula matunda mara kwa mara anza sasa.Hakikisha unakula matunda kila wiki na pia ni vyema ukala matunda mbalimbali(usile tunda lilelile kila wiki) ili upate virutubisho tofauit tofauti.
SOMA:Muda Sahihi wa kula Matunda


6.KULA CHAKULA BORA


Kula chakura bora ni jambo muhimu sana kuliko bora chakula,sehemu kubwa ya afya yako inaboreshwa na kile chakula unachokula kwani chakula hubeba virutubisho mbalimbali vya kujenga mwili wako.Unapokula bora chakula unajiweka katika nafasi ya kudhoofisha afya ya mwili wako na kupelekea kupata magonjwa.Ila unapoamua kula chakula bora unaupa mwili wako virutumbisho muhimu katika kukulinda dhidi ya magonjwa na kuwa mtu mwenye afya nzuri wakati wote.Hivyo unashauriwa kula vyakula mbalimbali vyenye virutubisho mabalimbali ili kuimarisha afya yako.


7.KUWA MSAFI MUDA WOTE


Kuwa katika hali ya usafi muda wote ni jambo la muhimu sana katika kuboresha afya yako.Ukiwa katika mazingira ambayo si safi,unajiweka katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali amabayo yataathiri afya yako.Hakikisha mazingira unayoishi yapo katika hali ya usafi muda wote,mwili wako upo katika hali ya usafi,mazingira ya unapokula yapo pia katika hali ya usafi.Ukifanya haya utajiepusha na magonjwa mengi na kuifanya afya ya mwili wako kuwa bora muda wote.

8. KUSOMA KITABU AU MAKALA ZA KUJIFUNZA


Usomaji wa vitabu na makala mbalimbali huleta faida kubwa sana katika afya ya akili yako na ubongo wako.Faida kama Kuongeza uwezo wa ubongo,Kupunguza msongo wa mawazo,Kuongeza uwezo wa kutunza kumbukumbu na uwezo mzuri wa kufikiri na kupambanua mambo.Pia utafiti uliofanywa katika sayansi ya kijamii na madawa imeonyesha kuwa kwa kuwa na tabia ya kusoma vitabu humuongezea mtu muda wa kuishi.Penda kusoma vitabu mbalimbali mara kwa mara  hata kwa dakika 30 kila siku ili kuboresha afya yako.


9.FUNGA KULA CHAKULA


Hali ya kufunga kula huleta faida nyingi katika mwili wako.Baadhi za faida ni kuimarisha afya ya ubongo,kuboresha kinga ya mwili,kuimarisha afya ya ngozi na kuishi kwa muda mrefu.Si lazima kufunga kila siku au tangu asubuhi mpaka jioni,unaweza funga mara moja kwa wiki au unaweza funga kutokula mlo mmoja iwe asubuhi,mchana au jioni.
SOMA:Umuhimu wa Kufunga Kula Kiafya

10. KUPUMZIKA VYA KUTOSHA


Kupumzika ni jambo muhimu sana ndio mana kazi hufanywa kwa siku tano hadi sita katika wiki ili siku zilizobaki upumzike.Hakikisha unapata usingizi wa kutosha.Mwili wako sio sawa na mashine kwamba unaweza fanya kazi masaa 24 kwa siku saba za wiki.Unapopumzika unaupa mwili nafasi ya kuzalisha nguvu mpya za kukusaidia kufanya majukumu yako kwa usahihi.Watu ambao hawapati muda wa kupumzika huweza kudhoofisha afya ya moyo.Amua sasa kuwa na muda mzuri wa kupumzika.


Ni matumaini yangu kuwa ukizifanya tabia hizi 10 kuwa sehemu ya tabia zako za kila siku,hakika afya yako itaimalika vya kutosha.Kumbuka sio lazima ufanye mambo haya yote siku moja bali fanya unaweza kwa siku na mengine weka malengo ya kuyatimiza kila wiki.

Kama umeipenda chapisho hili basi gonga NZURI  na  kwa maswali au maoni zaidi basi tuandikie baada ya andiko hili, na pia kama ungependa kusoma andiko jengine kama hili basi jisajili kwa kuweka anuani yako  kwenye linki ya SUBSCRIBE.

Pia waweza tuandikia kwa email yetu Kuafit08@gmail.com 
Kwa number yetu ya Tigo +255 653 009 477  
Instagram account yetu  (KUAFITI), Facebook-(kuafit)


About Unknown

Unknown
Recommended Posts × +

0 comments:

KUPUNGUZA UZITO KWA MAJI YA BARIDI

Watu wengi katika jamii hupendelea kuoga na maji ya moto katika majira yote ya hewa lakini kutokana na utafiti uliofanywa na wanasayansi kam...